Pata taarifa kuu
AFRIKA-SOKA

Mechi mbalimbali kupigwa Jumamosi na Jumapili kwenye viwanja mbalimbali Afrika

Mechi za mwisho, hatua ya makundi kufuzu robo fainali ya michuano ya klabu bingwa na Shirikisho barani Afrika zitachezwa Jumamosi na Jumapili katika viwanja mbalimbali barani Afrika.

Timu mbalimbali zinatarajia kujitupa uwanjani Jumamosi na Jumapili katika miji mbalimbali Afrika.
Timu mbalimbali zinatarajia kujitupa uwanjani Jumamosi na Jumapili katika miji mbalimbali Afrika. RFI/Pierre René-Worms
Matangazo ya kibiashara

Mechi za kila kundi zitachezwa kwa wakati mmoja, ili kuepusha uwezekano wowote wa kupanga matokeo.

Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini, ambayo tayari imefuzu katika hatua ya robo fainali, kutoka kundi A, itamaliza kazi ugenini dhidi ya Wydad Casablanca ya Morocco, mjini Rabat.

Wydad Casablanca ambayo ina alama saba sawa na ASEC Mimosas, inahitaji kushinda mechi hiyo ili kuongeza matumaini ya kusonga mbele, sawa na ASEC Mimosas ambayo itakuwa ugenini dhidi ya Lobi Stars ya Nigeria.

Esperance de Tunis ya Tunisia ambayo imeshafuzu pia kutoka kundi B, itakuwa ugenini kumenyana na FC Platinum ya Zimbabwe ambayo tayari imeshaondolewa.

Hata hivyo, kazi kubwa itakuwa kati ya Horoya ya Guinea na Orlando Pirates ya Afrika Kusini kwa sababu, tofauti kati ya klabu hizi mbili ni moja.

Horoya ina alama saba huku Orlando Pirates ikiwa na alama sita. Mshindi atafuzu, lakini Horoya ikipata sare itakuwa imefuzu.

Kundi C, CS Constantine ya Algeria, TP Mazembe ya DRC na Club Africain ya Tunisia, zote zina nafasi kubwa ya kusonga mbele.

TP Mazembe ambayo ina alama nane, itakuwa katika uwanja wake wa nyumbani mjini Lubumbashi kucheza na CS Constantine ambayo ina alama 10 huku Club Africain ambayo ina alama saba, ikichuana na Ismaily ya Misri ambayo imeshaondolewa katika michuano hii.

Mambo yapo hivyo pia katika kundi D, ambalo linaongozwa na JS Saoura ya Algeria kwa alama nane huku Al-Ahly ya Misri na AS Vita Club ya DRC zikiwa na alama saba, lakini Simba ya Tanzania ina alama sita.

JS Saoura watakuwa ugenini mjini Alexandria dhidi ya Al-Ahly huku Simba wakiwakaribisha AS Vita katika uwanja wao wa nyumbani, jijini Dar es salaam.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.