Chiheb Ellili ajiuzulu kama kocha wa Club Africain
Chiheb Ellili, amejiuzulu kama kocha wa timu ya Club Africain baada ya kufungwa na TP Mazembe mabao 8-0 katika mechi ya kundi C, kuwania taji la klabu bingwa barani Afrika.
Imechapishwa:
Mechi hiyo ilichezwa mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Lubumbashi, na alifikia uamuzi huu baada ya mahojiano na kituo cha redio cha Mosaique FM.
“Nawajibikia matokeo ya Jumamosi, lakini kwa heshima ya wachezaji nimeamua kuondoka,” amesema kocha Ellili.
Licha ya kuondoka, amewashukuru wachezaji aliosema walicheza kufa kupona lakini kwa bahati mbaya wakafungwa, matokeo ambayo amesema hayatafutika hivi karibuni.
Kabla ya kujiuzulu kwake, kocha Ellili amekuwa akifunza klabu hiyo tangu mwezi Oktoba mwaka 2018, baada ya kuchukua nafasi ya José Riga aliyefutwa kazi, baada ya miezi mitatu.