Afrika Kusini, Ethiopia na Ujerumani yaanza kwa kupata medali ya dhahabu
Afrika Kusini, Ethiopia na Ujerumani yamekuwa mataifa ya kwanza kushinda medali ya dhahabu katika mashindano ya riadha ya dunia ya vijana wasiozidi miaka 18, inayoendelea kwa siku ya pili leo katika uwanja wa Michezo wa Kasarani jijini Nairobi nchini Kenya.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Afrika Kusini inaongoza jedwali kwa medali mbili baada ya Tshenolo Lemao kutoka Afrika Kusini kuishindia nchi yake medali ya dhahabu katika mbio za Mita 100, huku raia mwenzake Retshidisitswe Mlenga akimaliza wa pili na kushinda medali ya fedha.
Nafasi ya tatu ilimwendea Tyreke Wilson aliyeishindia Jamaica medali ya shaba katika mbio hizo za Mita 100 kwa upande wa wavulana.
Abersh Minsewo kutoka Ethiopia, aliishindia nchi yake medai ya dhahabu katika mbio za Mita 3000 kwa wasichana, huku nafasi ya pili ikimwendea Mkenya Emmaculate Chepkirui. Mwiethiopia mwingine, Yitayish Mekonene alishinda medali ya shaba.
Mjerumani Selina Dantzler naye ameishindia nchi yake medali ya kwanza kwa kupata dhahabu katika mchezo wa kurusha kitupe chenye uzito wa Kilo 3.
Siku ya Alhamisi kutakuwa na fainali ya kuruka urefu, Long Jump kwa upande wa wavulana, kurusha kitufe cha uzito wa kilo tano kwa upande wavulana, kurusha mkuki wa gramu 700 kwa upande wa wanaume pia lakini fainali ya Mita 100 kwa upande wa wasichana.