Yanga SC yatinga hatua nyingine katika michuano ya CAF
Mabingwa wa zamani wa Ligi Kuu Tanzania Bara wamefanikiwa kusonga mbele katika mashindano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika kwa jumla ya mabao 3-2, licha ya kulala ugenini kwa mabao 2-1 dhidi ya BDF XI ya Botswana.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Timu ya Young Africans maarufu kama Yanga ndiyo timu pekee ya Tanzania iliyobakia katika michuano ya Shirikisho la Kandanda barani Afrika, CAF kwa mwaka 2015.
Yanga wameweza kusonga mbele kwa kuwaondoa BDF XI kwa kuwafunga jumla ya mabao 3-2.
Katika mchezo wa kwanza uliochezwa jijini Dar es Salaam wiki mbili zilizopita, Yanga ilifanikiwa kuichapa timu hiyo ya jeshi ya Botwasa kwa mabao 2-0, kabla ya jana kufungwa 2-1 mjini Gaborone, Botswana.
Timu hizi ziliporudiana mjini Gaborone, Botswana, Ijumaa usiku, BDF XI waliibuka na ushindi wa magoli 2-1.
Kwa matokeo hayo, Yanga imefanikiwa kutinga hatua inayofuata ya Kombe la Shirikisho barani Afrika kutoka kwenye mzunguko wa awali kwa kukutana na mshindi kati ya Sofapaka ya Kenya na Platnum ya Zimbabwe.
Timu ya Azam iliyopata ushindi mzuri wa mabao 2-0 dhidi ya El Mereikh ya Sudan, katika kinyang'anyiro cha klabu bingwa barani Afrika ilijikuta ikipoteza mchezo wa marudiano mjini Khartoum baada ya kulazwa mabao 3-0 na hivyo El Mereikh kufuzu kwa jumla ya mabao 3-2.
Timu nyingine za Tanzania Zanzibar za KMKM na Polisi zimejikuta zikitupwa nje ya michuano ya vilabu barani Afrika kwa kupoteza michezo yao.