Mapigano yapamba moto karibu na bandari ya Hudaydah, Yemen
Mapigano makali yameshuhudiwa kati ya waasi wa Kihouthi na muungano wa kijeshi, unaoongozwa na Saudi Arabia, katika bandari ya Hudaydah nchini Yemen.
Imechapishwa:
Kuendelea kushuhudiwa kwa mapiganano haya, kunahatarisha maisha ya mamilioni ya raia wa Yemen kwa sababu, misaada ya kibinadamu haiwezi kuingia nchini humo.
Bandari hiyo imekuwa ikidhibitiwa na waasi wa Kihouthi tangu mwaka 2014, lakini jeshi linaloongozwa na Saudi Arabia, linasema linalenga kupata ushindi dhidi ya waasi hao.
Umoja wa Mataifa umeelezea wasiwasi wake kuhusu mapigano yanayoendelea kwa lengo la kudhibiti bandari ya Hudaydah nchini Yemen, bandari ambayo ni tegemeo kwa ajili ya kufikisha misaada ya kibinadamu nchini humo.
Vyombo vya habari vinaeleza kuwa majeshi yanayounga mkono serikali inayotambuliwa kimataifa yakisaidiwa na Saudi Arabua wanashambulia bandari hiyo ya Hudaydah ambayo kwa sasa inashikiliwa na wahouthi wanaodaiwa kusaidiwa na Iran.
Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu Yemen Martin Griffiths amesema mapigano zaidi kwenye eneo hilo yatakuwa na madhara makubwa kwenye hali ya kibinadamu pamoja na kuzorotesha mashauriano ya kisiasa.