Vita nchini Syria vyaingia mwaka wa nane, maelfu wapoteza maisha
Vita vya Syria vimeingia mwaka wa nane, tangu vilipoanza tarehe 15 mwezi Machi mwaka 2011 wakati makundi ya upinzani yalipojitokeza kupambana na wanajeshi wa serikali kwa lengo la kumwondoa madarakani rais Bashar Al Assad.
Imechapishwa:
Assad ambaye amekuwa akiongoza nchi hiyo tangu mwaka 2000, licha ya vita hivyo amekataa kuondoka madarakani huku akipata uugwaji mkono mkubwa kutoka kwa serikali ya Urusi.
Takwimu za Umoja wa Mataifa zinaonesha kuwa kwa muda huo wote, watu zaidi ya 350, 000 wamepoteza maisha katika mapigano hayo huku mamilioni wakikimbilia katika mataifa mengine.
Watoto na wanawake ni miongoni mwa maelfu ya watu waliopoteza maisha katika vita hivi ambavyo hadi sasa haijafahamika vitamalizika lini.
Vita hivyo vimeingia mwaka wa nane, wakati huu mashambulizi makali kati ya jeshi la Syria linalosaidiwa na lile la Urusi limeendelea kupambana na wapiganaji wa upinzani katika ngome pekee inayosalia ya Mashariki mwa Ghouta.
Syria na Urusi zimekataa kutekeleza azimio la Baraza la Usalama kusitisha mapigano katika ngome hiyo ya upinzani.
Maelfu ya watu wamekwama katika ngome hiyo ya upinzani bila ya mahitaji muhimu ya kibinadamu kama chakula na dawa mambo ambayo yanataharisha maisha yao.