Mahakama Kuu ya Iraq yafutilia mbali kura ya maoni ya eneo la Kurdistan
Mahakama Kuu ya Iraq imefutilia mbali kura ya maoni ya eneo la Kurdistan na kusema kwamba ni kinyume na katiba ya nchi hiyo. Septemba 25 wakazi wa Kurdisatan walijitokeza kwa wingi na kupiga kura ya maoni kwa uhuru wa eneo lao.
Imechapishwa:
Matokeo ya kura hiyo yamefutwa, kwa mujibu wa chanzo cha mahakama kilichonukuliwa na shirika la habari la Reuter.
Mahakama Kuu ina mamlaka ya kutatua migogoro kati ya serikali kuu ya Iraq na maeneo mengine, kama vile Kurdistan.
Oktoba 29 kiongozi wa Kurdistan Massoud Barzani alijiuzulu kwenye nafasi hiyo na kusema kwamba haitaendelea kuongoza eneo hilo.
Hata hivyo Bw. Barzani alisema atasalia kuwa mpiganiaji wa Wakurdi na ataendelea kutetea mafanikio ya watu wa Kurdistan.
Zaidi ya asilimia 72 ya wapiga kura walioorodheshwa, sawa na watu milioni 3.3, walishiriki katika kura hiyo ya maoni na kura ya "ndiyo" ilishinda kwa asilimia 92.73 ya kura zilizopigwa, kwa mujibu wa Tume ya Uchaguzi na kura ya maoni ya eneo la Kurdistan.
Wapiga kura walitakiwa kupiga kura ya "Ndiyo" au "Hapana" kwa kura hiyo ya maoni.
Swali hapa ilikua kuamua kama eneo la Kurdistan na maeneo ya Kikurdi ya nje ya eneo la Kurdistan kuwa nchi huru."