Pata taarifa kuu
BURUNDI-CNL-UCHAGUZI-USALAMA

Wafuasi wa CNL washerehekea uteuzi wa Agathon Rwasa kuwania urais

Wafuasi wa chama kikuu cha upinzani nchini Burundi CNL, wameendelea kusherehekea uteuzi wa Aghathon Rwasa kupeperusha bendera ya chama hicho katika Uchaguzi Mkuu ambao umepangwa kufanyika mwezi Mei mwaka huu.

Kiongozi wa chama kikuu cha upinzani  cha CNL nchini Burundi, Agathon Rwasa.
Kiongozi wa chama kikuu cha upinzani cha CNL nchini Burundi, Agathon Rwasa. REUTERS/Thomas Mukoya
Matangazo ya kibiashara

Uamuzi huo wa kumteua Rwasa kupeperusha bendera ya chama cha CNL umefanywa na wajumbe wa chama hicho wakati wa mkutano mkuu wa chama cha CNL uliofanyika siku ya Jumapili jijini Bujumbura.

Rwasa anatarajiwa kupata ushindani kutoka kwa mgombea wa chama tawala CNDD-FDD, Evariste Ndayishimiye, mshirika wa karibu wa rais Pierre Nkurunziza ambaye hatawania urais, baada ya kuongoza nchi hiyo kwa mihula mitatu.

Aimé Magera, mwakilishi wa chama cha CNL nje ya nchi hiyo, amesema licha ya wafuasi wao kufungwa, kuteswa na kufanyiwa vitisho na baadhi kuuawa, chama cha CNL kiko tayari kushiriki uchaguzi wa urais, na wana imani kwamba watashinda uchaguzi huo.

Hali ya siasa nchini Burundi inaendelea katika hali ya mvutano kati ya chama tawala na upinzani, huku upinzani ukishtumu chama hicho kufanya kampeni wakati muda hauajawadia.

Hata hivyo baadhi ya wanasiasa waliofutwa katika chama cha CNDD-FDD ambao walikimbia nchi hiyo tangu mwaka 2015, kufuatia hatua ya rais Pierre Nkurunziza kuwania muhula watatu, wameanza kurejea nchini humo. Hivi karibuni, aliyekuwa kiongozi wa chama hicho tawala Jeremie Ngendakumana alirejea nchini, lakini mpaka sasa hajatangaza msimamo wake iwapo ataendelea na siasa au la.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.