Rwanda na Uganda waendelea kuboresha maridhiano
Nchi za Rwanda na Uganda zimekubaliana kubalishana wafungwa ikiwa ni mojawapo ya njia ya kuimarisha tena uhusiano kati ya nchi hizi mbli jirani.
Imechapishwa:
Hatua hii ilifikiwa baada ya mkutano kati ya rais wa Uganda Yoweri Museveni na rais wa Rwanda Paul Kagame, uliofanyika Jumapili Februari 2 jijini Luanda, nchini Angola, na kushuhudiwa pia na mwenyeji wao Joao Lourenco, na Felix Tshisekedi wa DRC.
Hata hivyo, haijafahamika ni lini wafungwa hao kutoka nchi hizo mbili wataachiliwa huru, huku wakikubaliana pia kuachana na vitendo vinavyoweza kurudisha nyuma juhudi za kupata amani ya kudumu.
Makubaliano ya kuondoa uhasama kati ya Rwanda na Uganda yaliyosainiwa na marais wa nchi hizo mbili, mwezi Agosti 2019, jijini Luanda nchini Angola yalileta afueni na furaha kubwa kwa raia wa nchi hizo, hususan wafanyabiashara.
Uganda imekuwa ikiishtumu Rwanda kwa kutumia raia wake kuhatarisha usalama wake, huku Rwanda nayo ikiishtumu Uganda kwa kuwatesa na kuwazuia raia wake, suala ambalo lililisababisha Kigali kufunga mpaka wake wa Katuna.
Uhusiano kati ya Rwanda na Uganda uliharibika mwezi Februari mwaka jana wakati Rwanda ilipofunga mpaka wake mkuu, kwa madai kuwa Uganda inawahifadhi wahalifu wa Rwanda, madai ambayo yalikataliwa na serikali ya Uganda.