Mwandishi wa habari Kabendera anayezuiliwa jela ampoteza mama yake Tanzania
Mama mzazi wa mwandishi wa habari nchini Tanzania Erick Kabendera anayezuiwa mahabusu, amefariki dunia. Familia yaka Kabendera imesema, Bi Verdiana Mjwahuzi mwenye umri wa miaka 80 alifariki dunia akiwa hospitalini jijini Dar es salaam.
Imechapishwa:
Wiki mbili zilizopita, mama huyo akiwa mwenye machozi, alizungumza na wanahabari akimwomba rais John Magufuli kumsamehe mtoto wake ambaye alisema ndio alikuwa tegemeo la familia hiyo.
"Mheshimiwa Rais na yeye ni mtoto kama walivyo watoto wengine hata kama ni mkubwa. Ni mzazi na analea watoto. Namwomba anionee huruma. Angalia maisha yalivyo magumu, dawa sipati. Naomba Rais anisaidie kama anavyosaidia wazazi wake," alisema Bi Verdiana.
Erick Kabendera alikamatwa mwezi Julai 2019 na kukabiliwa na mashtaka ya utakatishaji fedha, kukwepa kodi na kuongoza kikundi cha uhalifu. Mashtaka ambayo mawakili wake wameyakanusha.