Mafuriko yasababisha maafa Magharibi mwa nchi ya Uganda
Watu 12 wamepoteza maisha katika Wilaya ya Bundibugyo nchini Uganda baada ya kusombwa na maji, kutokana na mvua kubwa inayoendelea kunyesha na kusababisha mafuriko makubwa.
Imechapishwa:
Shirika la msalaba mwekundu nchini humo limethibitisha kupata miili ya watu hao ndani ya maji siku ya Jumamosi, kutokana na mafuriko hayo ambayo yameharibu pia miundo mbinu kama barabara.
Hali kama hii pia imekuwa ikishuhudiwa nchini Kenya na baadhi ya maeneo nchini Tanzania.
Watalaam wa hali ya hewa wanasema kuwa, eneo la Afrika Mashariki litaendelea kupokea mvua kubwa katika siku zijazo na kutoa wito kwa watu kuchukua tahadhari.
Maafisa nchini Kenya wanasema watu zaidi ya 120 wamepoteza maisha kutokana na mafuriko hayo makubwa ambayo yamewaacha watu wengine 160,000 bila makaazi.
Hali ilikuwa mbaya sana katika kaunti ya Pokot Magharibi kutokana athari ya mafuriko hayo.
Nchini Tanzania watu zaidi ya 40 wamepoteza maisha na wengine zaidi ya 1,000 kuyakimbia makwao katika miezi ya hivi karibuni.
Nchini za Burundi, Sudan, Djibouti, Ethiopia na Somalia pia zimeendelea kushuhudia mvua kubwa iliyosababisha mafuriko na maafa.