Watu nane wauawa Kaskazini mwa Rwanda baada ya kushambuliwa na watu wenye silaha
Watu wasiojulikana wenye silaha wametekeleza mauaji ya watu nane na kuwajeruhi wengine 18 usiku wa kuamkia Jumamosi, Kaskazini mwa nchi ya Rwanda.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Tangazo kutoka jeshi la polisi nchini humo, linasema tukio la mauaji hayo lilitokea katika tarafa za Kinigi na Musanze wilayani Musanze jimbo la Kaskazini mwa nchi hiyo.
Aidha, taarifa hizo zimeeleza kuwa watu wasiojulikana ndio waliotekeleza mauaji hayo katika kijiji cha Kaguhu tarafa ya Kinigi lakini pia yametekelezwa kwa wakati mmoja katika kijiji kingine cha Mufukuru kata ya Kabazungu tarafa ya Musanza.
Imebainika kuwa silaha zilizotumika katika kutekeleza mauaji hayo ni bunduki pamoja na zile za jadi.
Kwa mujibu wa shuhuda mmoja ameviambia vyombo vya habari Kaskazini mwa nchi hiyo ni kuwa, katika familia moja wauaji hao waliwauwa baba mmoja na vijana wake wawili.
Huu ni uvamizi wa tatu kufanywa katika kipindi cha mwaka mmoja ambapo mauaji ya awali yalifanywa katika vijiji vilivyo karibu na pori la Nyungwe kati ya Rwanda na Burundi.
Ripoti ya Mwandishi wetu wa Kigali, Bonaventure Chubahiro.