Pata taarifa kuu
BURUNDI-TANZANIA-UNHCR-WAKIMBIZI-USALAMA

Tanzania: Karibu wakimbizi wa Burundi 600 warudishwa nyumbani kwa hiari yao

Wakimbizi wa Burundi 600 waliokimbilia nchini Tanzania wamerudishwa makwao "kwa hiari yao" tangu Alhamisi, Oktoba 3, kwa mujibu wa serikali ya tanzania.

Basi lililokuwa limebeba wakimbizi wa Burundi 600 waliwasili kwenye mpaka wa Gisuru mkoani Ruyigi, Mashariki mwa Burundi, Oktoba 3, 2019.
Basi lililokuwa limebeba wakimbizi wa Burundi 600 waliwasili kwenye mpaka wa Gisuru mkoani Ruyigi, Mashariki mwa Burundi, Oktoba 3, 2019. © TCHANDROU NITANGA / AFP
Matangazo ya kibiashara

Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Wakimbizi, UNHCR, lilikuwa limemepanga katika siku za hivi karibuni kuwarudisha nchini Burundi wakimbizi takribani 400, wote kwa hiari yao.

Hata hivyo, wakimbizi 588 ndio walisafirishwa hadi katika kambi ya muda ya Nyabitare katika mkoa wa Ruyigi, mashariki mwa Burundi. UNHCR imehakikisha kwamba imechunguza kuwa "wale ambao waliongezwa katika kundi hilo la watu 400 wamerudishwa kwa hiari yao".

Tangu mwaka 2017, wakimbizi zaidi ya 78,000 kutoka Burundi wamerudishwa kutoka Tanzania.

Baada ya mkutano na mwenzake wa Burundi mwishoni mwa mwezi Agosti, Waziri wa Mambo ya Ndani wa Tanzania alitangaza kwamba serikali yake itawarudisha kwa hiari yao au kwa nguvu wakimbizi wote wa Burundi kuanzia tarehe mosi Oktoba mwaka huu. Uamuzi ambao ulikosolewa na jamii ya kimataifa.

Lakini siku ya Alhamisi asubuhi serikali ya Tanzania ilibadili msimamo na kurejelea kauli yake. Msemaji wa serikali ya Tanzania, Hassan Abbas, katika mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es salaam alibani kwamba "hakuna mkimbizi wa Burundi atalazimishwa kurudi nchini mwake, kama sio kwa hiari yake".

Katika kambi ya wakimbizi ya Nduta, Gérard, ambaye alitoroka nchi yake ya Burundi tangu kuzuka kwa mgogoro wa kisiasa mwaka 2015, amesema kuwa anafurahishwa na kauli hiyo ya serikali ya Tanzania, lakini ana matumaini kwamba "viongozi wa Tanzania hawatabadili tena kauli hiyo".

Wakimbizi 588 waliorudishwa nchini Burundi wanatarajia kusafirishwa hadi katika vijiji vyao leo Ijumaa. Bado kuna wakimbizi wa Burundi 225,000 nchini Tanzania, wakati maelfu ya Warundi wanaendelea kuitoroka nchi yao kila mwezi, kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Wakimbizi, UNHCR.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.