Rwanda kuanza kuwapokea wakimbizi kutoka nchini Libya
Kundi la kwanza la wakimbizi 75 waliokuwa wamezuiwa nchini Libya wakiwa njiani kwenda barani Ulaya, wanatarajiwa kupokelewa nchini Rwanda kuanzia siku ya Alhamisi.
Imechapishwa:
Hatua hii inakuja, baada ya Rwanda pamoja na Umoja wa Afrika na Tume ya Umoja wa Mataifa ya kutetea wakimbizi UNHCR, kuingia katika mkataba wa pamoja kuhusu wakimbizi hao.
Rais Paul Kagame akizungumza kwenye Mkutano Mkuu wa Umoja wa Matifa jijini New York nchini Marekani, ameelezea utayari wa nchi yake kuwakaribisha wakimbizi hao kutoka mataifa mbalimbali barani Afrika.
Awali, Rwanda imesema iko tayari kuwapa hifadhi wakimbizi 30,000.
Afisa wa juu wa Umoja wa Mataifa, amesema kuwa, kundi la kwanza la wakimbizi kutoka Libya wataanza safari kuondoka nchini humo siku ya Alhamisi, usiku.
“Kundi la kwanza la wakimbizi litaondoka nchini Libya, na wanatarajiwa kufika jijini Kigali Alhamisi usiku,” alisema afisa hiyo kupitia taarifa kupitia barua pepe.
“Wakimbizi zaidi wapatao 125, wanatarajiwa kuwasili nchini Rwanda kati ya tarehe 10 -12 mwezi Oktoka,” aliongeza.
Taarifa zinasema kuwa wakimbizi hao watapewa hifadhi chini Rwanda, kabla ya kwenda katika nchi nyingine.
Umoja wa Mataifa wanasema kuna wakimbizi 42,000 ambao wanazuiwa nchini Libya, baada ya harakati zao za kwenda barani Ulaya kutozaa matunda.