Maafisa nane wa polisi wauawa nchini Kenya baada ya gari lao kukanyaga bomu
Maafisa nane wa Polisi wameuawa katika kaunti ya Wajir nchini Kenya, karibu na mpaka na nchi ya Somalia baada ya gari walimokuwa wanasafiria kukanyaga bomu lililotegwa ardhini.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Inspekta Mkuu wa Polisi nchini humo Hilary Mutyambai amethibitisha kutokea kwa mlipuko huo na kusema kuwa waliotekeleza wanatafutwa.
Wakati wa shambulizi hilo, maafisa 11 wa polisi walikuwa ndani ya gari hilo wakipiga doria katika eneo hilo ambalo limeendelea kushuhudia vitisho vya usalama kutoka kwa kundi la Al Shabab.
Hata hivyo, kundi la Al Shabab halijajitokeza kudai kuhusika na shambulizi hilo.
Mwezi Juni mwaka 2018, maafisa wengine nane waliuawa baada ya kutokea kwa shambulizi lingine kama hili katika Kaunti hiyo.
Kaunti za Wajir, Mandera na Garissa yameendelea kulengwa na kundi la Al Shabab, huku maafisa wa usalama wakishambuliwa zaidi.
Kenya imeendelea kupata vitisho kutoka kwa kundi la kigaidi la Al Shabab nchini Somalia, baada ya kutuma jeshi lake nchini humo mwaka 2011 kwenda kupambana na kundi hilo.
Tangu mwaka 2007, kundi la Al Shabab limekuwa likiisumbua serikai ya Mogadishu na Umoja wa Afrika uliamua kutuma kikosi chake cha wanajeshi 20,000 kukabiliana na kundi hilo la kigaidi.