Pande hasimu Sudani Kusini kukutana kwa mazungumzo Ethiopia
Pande zinazohasimiana nchini Sudan Kusini zimepanga kukutana kwa mazungumzo leo Alhamisi jijini Addis Ababa, Ethiopia kujaribu kuokoa makubaliano ambayo yanaonekana kukwama siku chache kabla ya kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa.
Imechapishwa:
Mazungumzo ya Addis Ababa yanatarajiwa kuwaleta pamoja rais Salva Kiir, kiongozi wa waasi Riek Machar pamoja na makundi mengine yaliyotia saini mkataba wa amani wa mwezi Septemba mwaka jana.
Pande hizo zimekuwa zikivutana kuhusu namna ya kutekeleza baadhi ya vipengele vya mkataba wenyewe, likiwemo suala tata la usalama wa Riek Machar mjini Juba na uundwaji wa jeshi la kitaifa.
Taarifa ya Jumuiya ya Maendeleo ya nchi za Afrika Mashariki na Kati IGAD imesema jumuiya hiyo imelazimika kuitisha kikao hiki cha siku mbili ili kupata suluhu itakayowezesha kuundwa kwa Serikali ya kitaifa.
Juma lililopita Riek Machar alisema hayuko tayari kurejea Juba ikiwa usalama wake haujahakikishwa na kutaka zoezi la uundaji wa Serikali ya kitaifa lisogezwe mbele.