Mamia ya abiria wakwama kufuatia mgomo katika uwanja wa Kimataifa wa ndege jijini Nairobi
Shughuli za safari za ndege zimekwama katika Uwanja wa Kimataifa wa ndege wa Jomo Kenyatta jijini Nairobi nchini Kenya, baada ya wafanyikazi wanaotoa huduma mbalimbali katika uwanja huo kugoma.
Imechapishwa:
Mgomo huo ulianza saa tisa usiku, kwa kile wafanyikazi hao wanalalamikia uongozi wa usimamizi wa shughuli za usafiri katika uwanja huo.
Aidha, wanasema hawataki uonevu kuhusu namna wafanyikazi wanavyoajiriwa, marupurupuru, lakini pia wanapinga mpango wa serikali kukabidhi uwanja huo kwa Shirika la ndege nchini KQ, kuusimamia, wakihofia kupotea kwa ajira.
Mamia ya abiria wamekwama, huku Shirika la ndege nchini humo likiwaambia wateja wake kutofika katika uwanja huo kwa sababu hakuna kinachoendelea.
“Tunapenda kuomba radhi wateja wetu na umma kwa kinachoshuhudiwa kwa sababu ya mgomo huu haramu unaofanywa na wafanyikazi wa huduma za safari za angaa (KUWA), “ taarifa ya Shirikisho hilo imeeleza.
Abiria wengi, wameonekana kutojua la kufanya licha ya Waziri wa uchukuzi James Macharia kuwahakikishia kuwa changamoto inayojitokeza, itatuliwa baada ya mfupi.
“Nimekuwa hapa kuanzia saa tisa alfajiri, hakuna ndege yoyote, tumeambiwa tusubiri mawasiliano,” alisema Mercy Mwai mmoja wa abiria aliyezungumza na Shirika la Habari la Ufaransa AFP.
Viongozi wa Shirikisho la wafanyikazi hao wamekamatwa, baada ya serikali kusema kuwa mgomo huo ulikuwa haramu baada ya Mahakama kutoa agizo huku polisi wa kupambana na ghasia wakitumia mabomu ya machozi kuwasambaratisha wafanyikazi hao na baadhi ya abiria kujeruhiwa.