Magari kutoruhusiwa katikati ya jiji la Nairobi mara mbili kwa wiki
Serikali ya Kenya imetangaza kuwa, kila siku Jumatano na Jumamosi kuanzia mwezi Februari, hakuna magari yatakayoruhusiwa kufika katikati ya jiji kuu, Nairobi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wizara ya Uchukuzi imesema lengo ni kuondoa msongamano mkubwa wa magari lakini pia, kutoa nafasi kwa mabasi maalum kuanza kuwasafirisha abiria katika maeneo ya jiji kuu.
Mpango huu umechelewa kuanza kutekelezwa kutokana na mvutano wa ni nani atahusika na usimamaizi wa mabasi hayo maalum kati ya serikali na wamiliki wa magari ya umma, maarufu kama matatu nchini humo.
Mpango huo utakapoanza kutekelezwa, watu wanaomiliki magari watayaacha nyumbani au eneo maalum ya kuyaegesha na kuabiri mabasi maalum kuingia katikati ya jiji.
Wachuuzi wana la kufurahi kutokana na mpango huu kwa sababu watapewa nafasi ya kuuza bidhaa zao katika baadhi ya barabara za jiji hilo.
Waziri wa Uchukuzi James Macharia amesema mabasi zaidi ya sitini yamenunuliwa kutoka Afrika Kusini ili kuanza kutekeleza mradi huo.