Chama tawala nchini Tanzania, kumhoji kada wake Benard Membe
Chama kinachotawala nchini Tanzania, Chama cha Mapinduzi (CCM) kimemwita kwa mahojiano kada wake, Benard Membe kwa madai ya kumkwamisha Rais John Magufuli.
Imechapishwa:
Membe, mwanasiasa aliyefikia viwango vya juu nchini humo alikuwa Waziri wa Mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa katika serikali ya awamu ya nne, iliyoongozwa na Jakaya Mrisho Kikwete.
Ripoti zilizochapishwa na vyombo vya habari nchini Tanzania zinasema kauli ya kuitwa na kuhojiwa imetolewa na Katibu Mkuu wa chama hicho Dr.Bashiru Ally akiwa Mkoani Geita, kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.
"Namhitaji sana Membe, ningekuwa na namba yake ningempigia. Sikumsema Membe kama mwanachama maarufu bali kama mwanachama wa kawaida kama wanachama wengine,"amekuliwa na mtandao wa gazeti la kila siku la Mwananchi
Tangu aliposhindwa na Dr. John Magufuli katika kinyang'anyiro cha kutafuta mgombea wa CCM katika uchaguzi wa 2015, Membe amekuwa akionekana kwa nadra sana hadharani lakini bado anatajwa kama mwanachama mwenye ushawishi ndani ya chama tawala.
Ripoti zaidi zinasema Membe ameitia wito wa kuonana na Katibu Mkuu Dr. Bashiru Ally na amesema pindi atakaporejea Tanzania ataonana na kiongozi huyo.
Baadhi ya magazeti nchini humo yamekuwa yakiripoti habari za kumhusisha mwanasiasa huyo kuratibu mpango wa kumkwamisha rais Magufuli na kutengeneza mazingira ya kuwania urais kupitia CCM mwaka 2020.