Makongoro Mahanga:Niliongoza Jimbo la Ukonga kwa miaka 10, kwa kuiba kura
Mwanasiasa wa upinzani nchini Tanzania, Dr. Makongoro Mahanga amesema aliongoza Jimbo la uchaguzi la Ukonga, kutokana na wizi wa kura.
Imechapishwa:
Mahanga ametoa kauli hiyo wakati akishiriki mkutano wa kisiasa katika Jimbo la Ukonga, wa kumnadi mgombea ubunge wa Chadema Asia Msangi.
Kiongozi huyo alikuwa mbunge katika Jimbo la Ukonga kwa miaka 10 kwa tiketi ya Chama tawala CCM, mwaka 2015 alijiunga na Chama Kikuu cha Upinzani cha Chadema.
Hata hivyo, Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Uhusiano wa Kimataifa, Kanali Ngemela Lubinga ametupilia mbali matamshi ya mwanasiasa huyo, akisema anadhalilisha elimu yake.
"Huwezi kudeal na mtu kama huyo, yaani anawaambia wananchi kuwa aliiba kura? Ili iweje?."Kanali Lubinga, amenukuliwa na gazeti la kila siku la Mwananchi
Uchaguzi mdogo katika Jimbo la Ukonga utafanyika Septemba 16 baada ya aliyekuwa mbunge wake Mwita Waitara kuhamia CCM. CCM imemsimamisha Waitara kugombea nafasi hiyo.