Pata taarifa kuu
SUDANI-KUSINI-MAZUNGUMZO-SIASA-USALAMA

Rais wa Sudan Salva Kiir na kiongozi wa waasi Riek Machar wakubali kuweka kando tofauti zao

Viongozi wa Afrika Mashariki walikutana huko Addis Ababa Jumatano wiki hii, ili kuhimiza mchakato wa amani nchini Sudan Kusini, kufuatia mkutano kati ya Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir na kiongozi wa waasi Riek Machar. Mkutano ambao ni wa kwanza tangu miaka miwili iliyopita.

Rais wa Sudani Kusini Salva Kiir (kushoto) na kiongozi wa waasi Riek Machar (kulia).
Rais wa Sudani Kusini Salva Kiir (kushoto) na kiongozi wa waasi Riek Machar (kulia). REUTERS/Goran Tomasevic
Matangazo ya kibiashara

Wawili hao walikutana Jumatano usiku wiki hii, katika mji mkuu wa Ethiopia, Addis Ababa, baada ya kualikwa na Waziri Mkuu wa nchi hiyo Abiy Ahmed, ambaye kwa sasa ni mwenyekiti wa Jumuiya ya Uchumi na Maendeleo Afrika Mashariki (Igad), ambayo kwa miezi mingi ilikua ikisimamia na kutaka kuanzishwa upya kwa mchakato wa amani nchini Sudani Kusini.

Mada ya mazungumzo yao haikuweza kuwekwa wazi, lakini picha za mkutano huo zinaonyesha Salva Kiir, Riek Machar na Abiy Ahmed wakizungumza wakiwa watatu, huku tabasamu zikiwajaa.

Kwa mujibu wa Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed kupitia picha za video mtandaoni anaonekana kukumbatiana kwa pamoja na viongozi wawili akisikika akisema "nafurahi kuona viongozi hawa wamekubali kuwaunganisha wananchi na kuweka kando tofauti zao kwa ajili ya amani ya Sudan Kusini."

Bado hata hivyo hawajatoa taarifa ya pamoja.

Salva Kiir na Riek Machar walikutana kwa mara ya mwisho mnamo mwezi Julai 2016, saa chache kabla ya mapigano makubwa kuzuka katika mji wa Juba kati ya majeshi yao.

Mapigano hayo yalisababisha kiongozi wa waasi kukimbia nchi hiyo, na alieleza kushindwa kwa makubaliano ya amani yaliyofikiwa mnamo mwezi Agosti 2015 ambayo yaliruhusu Bw Machar kuteuliwa kwenye nafasi ya makamu wa rais.

Viongozi wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Uchumi na Maendeleo (Igad)- ikiwa ni pamoja na rais wa Sudan Omar al-Bashir, Uhuru Kenyatta wa Kenya, rais wa Somalia Mohamed Abdullahi Mohamed - watajaribu kuongeza ushawishi wao kwa Salva Kiir na Riek Machar ili kuanzisha upya mchakato wa amani uliosimama.

Mgogoro wa Sudan Kusini, uliozuka mnamo mwezi Desemba 2013, miaka miwili baada ya nchi hiyo kupata uhuru wake, umesababisha maelfu ya watu kupoteza maisha, karibu watu milioni nne kutoroka makaazi yao (kwa jumla ya wakazi milioni 12 wa nchi hiyo) na kusababisha mgogoro mkubwa wa kibinadamu.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.