Magufuli: Tunataka Bunge letu kuzingatia umuhimu wa sekta za usafiri na nishati
Rais wa Tanzania amelitaka bunge la jumuiya ya Afrika mashariki kuzingatia umuhimu wa sekta za usafiri na nishati, miongoni mwa nyengine, kama nguzo muhimu za maendeleo ya jumuiya hiyo.
Imechapishwa:
Akihutubia Bunge la Afrika Mashariki (EALA) siku ya Jumanne wiki hii mjini Dodoma kwa mara ya kwanza tangu aingie madarakani alitilia mkazo matumizi ya rasilimali zilizopo katika jumuiya kama vile madini, na nyingine, ili kunufaisha wananchi wa ukanda huu kwani kutokufanya hivyo kunaigharimu jumuiya.
Rais Magufuli amesema kuendelea kutumia bidhaa kutoka nje ya jumuiya ni kuendelea kufaidisha mataifa mengine wakati mataifa ya Afrika mashariki yakikabiliwa na umasikini.
Kwa upande wake spika wa bunge la Afrika mashariki Dokta Martin Ngoga amesema kwa sasa hakuna sababu kuendelea kutumia lugha za kigeni wakati Lugha ya kiswahili inazungumzwa katika nchi za jumuiya.
Viongozi wengine waliohudhuria bungeni hapo ni Naibu wa Pili wa Waziri Mkuu wa Uganda Kirunda Kivejinja, Mawaziri, Mabalozi wanaowakilisha nchi mbalimbali nchini Tanzania.