Wanajeshi wa kulinda amani waongezewa mwaka mmoja nchini Sudan Kusini
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limepitisha kwa kauli moja azimio linaloruhusu jeshi la kulinda amani la Umoja wa Mataifa kuendelea kuwa nchini Sudan Kusini kwa muda wa mwaka mmoja zaidi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Umoja wa Mataifa umetuma wanajeshi wake 17,000 kuwalinda raia jijini Juba baada ya kuzuka kwa vita kati ya wanajeshi wa serikali na vikosi vya aliyekuwa makamu wa rais na kiongozi wa waasi Riek Machar mwaka 2015.
Aidha, wajumbe hao wametishia kuiwekea Sudan Kusini vikwazo vya kutonunua silaha kutoka nje ya nchi iwapo vita vitaendelea kushuhudiwa katika taifa hilo.
Lengo la azimio hilo lililowasilishwa na Marekani,ili kuishinikisha serikali ya rais Salva Kiir kushiriki katika mzunguko mwingine wa mazungumzo ya amani mwezi ujao jijini Addis Ababa nchini Ethiopia.
Marekani imekuwa ikiilaumu serikali ya Sudan Kusini kwa kushindwa kuheshimu mikataba ya amani na kuendeleza vita katika taifa hilo.
Vita nchini Sudan Kusini vimesababisha maelu ya watu kupoteza maisha na wengine kuyakimbia makwao.