Wadau katika mazungumzo ya amani ya Burundi washindwa kuafikiana
Baada ya kuahirishwa mara kadhaa, hatimae hapo jana mkutano wa hadhara wa wajumbe katika mazungumzo ya kusaka suluhu ya mgogoro wa Burundi yanayoendelea huko Arusha umefanyika na kudumu dakika 45, huku kukiwa na maskitiko ya kutopiga hatuwa chanya.
Imechapishwa:
Muwezeshaji katika mazungumzo hayo rais wa zamani wa Tanzania Benjamin Mkapa amekutana na wajumbe wote katika mazungumzo hayo tangu yalipoanza Juma lililopita.
Katika Hotuba yake Benjamin Mkapa amewaeleza wajumbe katika mazungumzo hayo kwamba anasikitishwa kuona hakuna hatua chanya iliopigwa hadi sasa tangu kuanza kwa mazungumzo hayo Novemba 28.
Kwa kipindi cha siku kadhaa wajumbe katika mazungumzo wamejadili kuhusu pointi nane zilizowekwa mezani ambazo zilipendekezwa na jopo la muwezeshaji lakini imekuwa vigumu kupiga hatua.
Kwa mujibu wa muwezeshaji Benjamin Mkapa, wajumbe hao walitakiwa kukutana kwa pamoja na kuanza kujadiliana mambo yanayo watofautisha. Lakini sasa, ujumbe wa serikali ya Burundi, chama tawala na washirika wake wote, wamekataa kutia bidii katika kushiriki katika kile wanachokiona kama mazungumzo na upinzani wa ndani, uliopo Arusha,
Badala yake wameendelea kushikilia msimamo wao, hakuna mazungumzo, na hatua itayofuata ifanyike Burundi huku wakidai haki ya serikali ya sasa kufanya mabadiliko ya katiba wakati huu wakisisitiza kuwa kila kitu kinakwenda sawa.
Kutokana na hali hiyo, muwezeshaji Benjamin Mkapa hazungumzi tena juu ya majadiliano kabla yakufikia makubaliano ambayo yatasainiwa mbele ya wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika mashariki hapo Ijumaa, Desemba 8.
Upinzani wa ndani katika mazungumzo hayo, ulitaraji mazungumzo ya kweli, lakini sasa wamekata matumaini na kusema kwamba kinachoendelea ni dhahiri kuwa yamefeli.