Marekani yatoa wito wa mazungumzo ya kitaifa nchini Kenya
Marekani imetoa wito wa kufanyika kwa mazungumzo ya kitaifa nchini Kenya baada ya kuapishwa kwa rais Uhuru Kenyatta kuongoza Kenya kwa muhula wa pili siku ya Jumanne.
Imechapishwa:
Taarifa kutoka Washington DC, imeeleza kuwa mazungumzo ndio njia pekee ya kutafuta mwafaka wa kisiasa ambao umewagawa wananchi wa taifa hilo la Afrika Mashariki baada ya kumalizika kwa Uchaguzi wa urais wa mwezi Agosti uliosusiwa na upinzani.
Aidha, taifa hilo limesema litaendelea kushirikiana na viongozi wa nchi hiyo kuimarisha uhusiano wa nchi hizo mbili miongini mwa mambo mengine muhimu.
Wito kama huo umetolewa na serikali ya Uingereza kupitia Waziri wa Masuala ya Afrika Rory Stewart aliyehudhuria kuapishwa kwa Kenyatta.
Stewart amempongeza rais Kenyatta na Naibu wake William Ruto na kutoa wito kwa Wakenya kupiga hatua baada ya kumalizika kwa kipindi cha kisiasa.
Rais Kenyatta katika hotuba yake alisema atatumia kila mbinu kikatiba kuiweka nchi hiyo pamoja.
Naye kiongozi wa upinzani NASA Raila Odinga amekataa kumtambua rais Kenyatta kama kiongozi halali wa nchi hiyo na kusema kuwa ataapishwa tarehe 12 mwezi Desemba.