WFP yapunguza mgao wa chakula kwa wakimbizi kutoka kambi 3 Tanzania
Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani WFP, limelazimika kupunguza mgao wa chakula kwa wakimbizi laki 3 na elfu 20 wanaoishi katika kambi za Mtendeli, Nduta na Nyarugusu mkoani Kigoma kaskazini magharibi mwa Tanzania.
Imechapishwa:
WFP inasema imelazimika kufanya hivyo kwa sababu ya upungufu wa fedha.
WFP inasema inahitaji kwa haraka jumla ya Dola za Marekani milioni 23.6 kuanzia sasa hadi Desemba, 2017 ili imudu kuendelea kutoa mgao unaokidhi mahitaji ya chakula na lishe kwa wakimbizi wanaoishi nchini Tanzania.
Michael Dunford, mwakilishi mkaazi wa shirika la WFP nchini Tanzania, amesema shirika lake haliwezi kuwahudumia ipasavyo wakimbizi hao hadi pale watakapopata fedha.
Raia wengi wa Burundi waliokimbilia nchini Tanzania walikimbia nchi yao kutokana na vurugu zilizotokea baada ya rais Pierre Nkurunziza kuwania urais kwa muhula wa tatu.
Mgogoro huo umesababisha vifo vya watu zaidi ya 1,000 na maelfu kukimbilia nje ya nchi.