Machar akataa kuwaamuru waasi kuacha vita dhidi ya Juba
Kiongozi wa waasi nchini Sudan Kusini Riek Machar amekataa kuwaambia waasi anaowaongoza kuacha mapigano dhidi ya vikosi vya serikali ya Juba, ili kushiriki katika mazungumzo ya amani na rais Salva Kiir.
Imechapishwa:
Rais wa zamani wa Bostwana Festus Mogae ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya kuthathmini wa mkataba wa amani uliotiwa saini mwaka 2015 kati ya Machar na rais Salva Kiir, ameliambia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuwa alimtembelea Machar anayeishi nchini Afrika Kusini.
Mogae amesema, Machar alimwambia wazi wazi kuwa hawezi kuagiza kusitishwa kwa mapigano yanayoendelea licha ya kumshauri kufanya hivyo.
Aidha, Mogae amesema, Machar amemwambia kuwa anataka kuwepo kwa mazungumzo mapya ya kisiasa ambayo angependa yafanyike nje ya Sudan Kusini.
Mapigano nchini humo ambayo yamekuwa yakiendelea nchini Sudan Kusini tangu mwaka 2013 na kuvunjika kwa serikali iliyoundwa baada ya kupatikana kwa uhuru mwaka 2011.
Maelfu ya raia wa Sudan Kusini wamepoteza maisha na wengine kuyakimbia makwao kwa sababu ya vita hivi vinavyoendelea.
Juhudi za mataifa ya Afrika Mashariki IGAD, kujaribu kutatua mzozo huu hazijafua dafu.