Kenya: Jubilee na NASA kuzindua Ilani zao kuelekea Uchaguzi Mkuu
Vyama vikuu vya siasa nchini Kenya Jubilee na Muungano wa upinzani NASA vinazindua Ilani zao leo na kesho jijini Nairobi, kuelekea Uchaguzi Mkuu tarehe 8 mwezi Agosti.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Leo ni zamu ya chama tawala cha Jubilee cha rais Uhuru Kenyatta anayewania urais kwa muhula wa pili, kuwaambia Wakenya wanachopanga kuwafanyia kwa muda wa miaka mitano ijayo ikiwa watashinda Uchaguzi huu.
Kenyatta anatafuta ungwaji mkono akiwa na rekodi ya kujenga reli ya kati iliyozinduliwa mwezi uliopita, kuongeza usambazaji wa nguvu za umeme kwa idadi kubwa ya raia wa nchi hiyo wanaoishi vijijini na kuimarisha miundo mbinu kama ujenzi wa barabara.
Hata hivyo, gharama ya kupanda kwa maisha iliyosababisha bei ya vyakula kuongezeka na ukosefu wa unga wa mahindi, kashfa mbalimbali za ufisadi na kushindwa kukabiliana na kundi la kigaidi Al Shabab kutoka nchini Somalia wakati wa uongozi wake ni masuala ambayo yanaonekana kuwapa changamoto kubwa.
Naye mgombea wa urais kupitia NASA Raila Odinga, kesho anatarajiwa kutoa ahadi za kupunguza gharama za maisha, kupambana na ufisadi na kufanikisha serikali za Kaunti kwa kuhakikisha kuwa serikali kuu inatoa fedha za kutosha kuendeleza maendeleo mashinani.
Upinzani katika mikutano yake ya kisiasa, unawaambia Wakenya kuwa serikali ya rais Uhuru Kenyatta haistahili kuchaguliwa tena kwa sababu imeshindwa kutekeleza ahadi zake kama kutoa vipatakalishi kwa wanafunzi wa darasa la kwanza miongoni mwa ahadi nyingine walizotoa mwaka 2013.
NASA inasema huu ndio mwaka wa ukombozi wa mwisho wa taifa hilo.
Hata hivyo, wachambuzi wa siasa nchini Kenya wanasema kuwa, kwa kiasi kikubwa uzinduzi wa Ilani hizi hazitaleta mabadiliko kwa wapiga kura nchini humo kwa sababu Wakenya hupiga kura kwa misingi ya majimbo na ukabila.