Ruto: Tutawafukuza ndani ya Jubilee watakaopinga sheria ya kuhamahama vyama
Wakati nchi ya Kenya ikijiandaa kwa uchaguzi mkuu wa mwakani, muungano wa chama cha Jubilee, umewaonya wanasiasa wake ambao hawataunga mkono muswada wa mabadiliko ya sheria inayokataza wanasiasa kuhamahama vyama.
Imechapishwa:
Akizungumza mara baada ya kukutana na sehemu ya wabunge wa Jubilee, kwenye ikulu ya Nairobi, naibu wa rais wa Kenya, William Ruto, amesema muungano wao umekubaliana kuwafurusha ndani ya chama chao kipya, wabunge ambao watapinga sheria hiyo.
Hata hivyo mapendekezo ya sheria hiyo yalikutana na upinzani mkali bungeni, ambapo asilimia kubwa ya wabunge walitaka kipengele kinachokataza wanasaisa kuhamahama vyama kifutwe kutoka kwenye ripoti ya kamati iliyoundwa kufanyia marekebisho tume ya uchaguzi nchini Kenya.
Hii leo bunge la kitaifa litaendelea na mjadala kuhusu kipengele hicho kabla ya kuamua kukifuta ama kuipitisha ripoti ya kamati na kipengele chenyewe bila kuifanyia marekebisho, suala ambalo wabunge wa Jubilee wamesema watapiga kura ya ndio kuidhinisha ripoti hiyo bila mabadiliko.
Kamati maalumu ya bunge iliyokuwa imeundwa kufanyia marekebisho tume ya uchaguzi nchini Kenya, ilipendekeza kutungwa kwa sheria itakayokataza wanasiasa kuhamahama vyama wakati wa uchaguzi mkuu, ambapo kamati hiyo ilitaka pendekezo hilo lipitishwe bila kupingwa.