Rais Kenyatta atangaza kuundwa kwa chama kipya kuelekea uchaguzi wa 2017
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta na Naibu wake Willima Ruto wametangaza rasmi kuwa chama kipya cha siasa cha Jubilee, kinacholeta pamoja vyama vinavyoiunga mkono serikali, kitazinduliwa rasmi mwezi ujao.
Imechapishwa:
Vyama mbalimbali ambavyo vimekuwa vikishirikiana na serikali ya rais Uhuru Kenyatta, vimeamua kuungana na kuunda chama kimoja kuelekea uchaguzi Mkuu mwaka ujao.
Rais Kenyatta ambaye anatarajiwa kutetea wadhifa wake mwaka ujao, amesema chama hicho kipya kitazinduliwa rasmi wakati wa mkutano Mkuu wa vyama mbalimbali jijini Nairobi, tarehe 9 na 10 mwezi ujao.
Uchaguzi wa mwaka 2013, rais Kenyatta akiwa kiongozi wa chama cha TNA, aliungana na William Ruto ambaye amekuwa kiongozi wa chama cha URP na kuunda muungano wa Jubilee.
Rais Kenyatta amesema chama hiki kitasaidia kupambana na siasa za kikabila nchini humo lakini pia kuimarisha umoja wa kitaifa na ametoa wito kwa wakenya kuwa wanachama.
Hata hivyo, muungano wa upinzani CORD unaoongozwa na Raila Odinga, na ambao pia unaundwa na vyama mbalimbali haujasema ikiwa nao utaunda chama kimoja kuelekea uchaguzi Mkuu mwaka ujao.