Iran imekata huduma ya Internet kabla ya maandamano mapya
Mamlaka nchini Iran imekata mawasiliano ya mitandao ya kijamii kupitia simu za mkononi katika majimbo kadhaa, shirika la habari la serikali ILNA limeripoti.
Imechapishwa:
Wakati huo huo serikali ya Iran imeonya wale wanaotumia mitandao ya kijamii kuhamasisha maandamano.
Hayo yanajiri wakati waandamanaji wameapa kuendelea na maandamano leo Alhamisi.
Vyombo vya habari vinavyodhibitiwa na serikali pia vimeripoti kwamba silaha 126 zilizotengenezwa nchini Marekani ambazo zimeingia nchini kinyume cha sheria kutoka nchi za kigeni, zimegunduliwa katika mji wa Isfahan, katikati mwa nchi.
Maandamano hayo yalisababishwa kwanza mnamo mwezi Novemba na kuongezeka kwa bei ya petroli, lakini madai ya waandamanaji sasa ni mengi ikiwa ni pamoja na suala la uhuru wa kisiasa.
Iran, ambayo imeendelea kukandamiza maandamano hayo, inashutumu 'majambazi' wenye mafungamano na watu waliokimbilia uhamishoni katika nchi za kigeni na nchi maadui - Marekani, Israeli na Saudi Arabia - kuchochea machafuko kwenye mitandao ya kijamii.