Hong Kong yaendelea katika hali ya sintofahamu
Wananchi wa mji wa Hong Kong wanajiandaa kwa maandamano makubwa yanayotarajiwa kufanyika kuanzia leo, ikiwa ni maandamano mfululizo ya karibu miezi mitatu, huku waandamanaji wanaopigania Demokrasia wakionesha kutokata tamaa.
Imechapishwa:
Maandamano ya hivi leo yatashuhudia wahasibu wakiandamana mbele ya ofisi za Serikali ambapo wataungwa mkono na mamia ya waandamanaji waliopanga kujitokeza kwenye maeneo mbalimbali ya mji wa Hong Kong.
Taarifa iliyotolewa na viongozi wa maandamano hayo, imesema wamepanga kutatiza shughuli za usafiri katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa mji huo pamoja na usafiri wa reli.
Uwanja wa ndege wa Hong Kong, ambapo ni moja ya viwanja vyenye shughuli nyingi duniani, juma lililopita ulisimamisha safari nyingi za ndege baada ya waandamanaji kuingia ndani ya uwanja.
Maandamano haya ambayo yalishika kasi mwezi Juni baada ya utawala wa Hong Kong kusitisha mjadala wa muswada tata wa kubadilishana watuhumiwa na Beijing, yamegeuka kuwa ya kupigania demokrasia na uhuru.