Putin amwalika Kim Jong-un kuzuru Urusi mwezi Septemba
Rais wa Urusi Vladimir Putin amemualika kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un kuzuru Urusi mnamo mwezi Septemba, msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov amesema Jumatatu wiki hii.
Imechapishwa:
Taarifa hiyo ilikuwa imeripotiwa na shirika la habari la Urusi RIA, likimnukuu mmoja wa manaibu spika wa baraza la wawakilishi, Ivan Melnikov.
Moscow imetoa pendekezo kwa Kim Jong-un kuhudhuria mkutano wa Uchumi wa nchi kutoka Mashariki utakaofanyika mnamo mwezi Septemba huko Vladivostok, Mashariki mwa Urusi.
Maeneo mengine na tarehe pia zinajadiliwa, kwa mujibu wa RIA.
Mwaliko huo ulitumwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi Sergei Lavrov, ambaye alizuru Pyongyang wiki iliyopita.
Kremlin pia imesema kuwa haikuwa na taarifa kutoka wa White House kuhusu kufanyika kwa mkutano kati ya Putin na Donald Trump tangu wawili hawa walipozungumza kwa njia ya simu mwezi Machi mwaka huu.
"Tunaona kuwa hakuna jitihada zozote zile (kutoka Marekani)," amesema Dmitry Peskov.
Gazeti la The Wall Street Journal limeripoti siku ya Ijumaa kuwa White House imeanza kufanya maandalizi ya mkutano wa kilele wa Putin-Trump.
Kim Jong-un na Donald Trump wamepanga kukutana Juni 12 huko Singapore.