Mkutano wa kihistoria kati ya Trump na Kim kufanyika Juni 12 Singapore
Rais wa Marekani Donald Trump ametangaza kuwa atakutana na Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un tarehe 12 mwezi Juni nchini Singapore.
Imechapishwa:
Itakuwa mara ya kwanza kwa rais wa Marekani kuwahi kukutana na kiongozi wa Korea Kaskazini, katika mkutano wa kihistoria ambao unatarajiwa kujadili namna ya Korea Kaskazini kuachana na mradi wake wa nyuklia.
Akiwa katika mkutano wa hadhara katika jimbo la Indiana rais, Trump amesema, ana matumaini makubwa kuwa mkutano huo utasaidia kuleta amani na usalama duniani.
Trump ametangaza hilo saa chache baada ya kuwapokea nyumbani raia watatu wa Marekani waliokua wakizuiliwa na Korea Kaskazini ambao waliachiliwa huru na kuruhusiwa kurejea nyumbani.
Mnamo mwezi Aprili mwaka huu Donald Trump alitangaza kwamba amekubali mwaliko wa kukutana moja kwa moja na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jon-un.
Haijafahamika ni kwanini Singapore imeteuliwa kuwa mwenyeji wa mkutano huo.