China kutuma mjumbe wake Korea Kaskazini baada ya ziara ya Trump Asia
China imetangaza kumtuma "mwakilishi maalum" nchini Korea Kaskazini siku ya Ijumaa, siku moja tu baada ya ziara ya Rais wa Marekani Donald Trump barani Asia, Rais Trump aliiomba China kuongeza shinikizo kwa Pyongyang.
Imechapishwa:
Mjumbe huyu wa Rais Xi Jinping, Song Tao, atahusika na kutoa taarifa kwa Pyongyang kuhusu maendeleo yanayohusiana na miaka mitano ya Mkutano Mkuu wa Chama cha Kikomunisti (CCP) uliofanyika katikati ya mwezi Oktoba, shirika la habari la serikali ya China, Xinhua, limearifu, bila kutoa maelezo zaidi.
Taarifa hii imethibitishwa na shirika la habari la Korea Kaskazini ,KCNA.
Uhusiano wa kidiplomasia kati ya China na Pyongyang unaendelea kukumbwa na jinamizi kufuatia mpango wa nyuklia wa Korea Kaskazini, na Xi Jinping hajakutana na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-Un, tangu Jong-Un kuingia madarakani mwishoni mwa mwaka 2011.
Kutumwa kwa Song Tao, pia mkuu wa "ofisi ya ushirikiano wa kimataifa" ya chama cha CCP, itakuwa ziara ya kwanza kwa viongozi wa juu wa China tangu ziara ya Naibu Waziri wa Mambo ya Nje Liu Zhenmin mnamo mwezi Oktoba 2016.
Tangazo la China linakuja siku moja baada ya Donald Trump kuhitimisha ziara yake ya siku 12 barani Asia, ambapo alionya kwamba "muda unakwenda" dhidi ya matarajio ya kijeshi ya Pyongyang.