Zaidi ya watu 750 wapoteza maisha kufuatia mafuriko kusini mwa Asia
Mafuriko na maporomoko ya ardhi yaliyosababishwa na mvua kubwa zinazoendelea kwa wiki moja katika bara la Asia yamesababisha vifo vya zaidi ya watu 750 katika nchi za Nepal, India na Bangladesh, kwa mujibu wa ripoti ya muda ya viongozi, iliyotolewa siku ya Jumatatu, Agosti 21. Na India ni nchi iliyoathirika zaidi.
Imechapishwa:
Zaidi ya miili hamsini iligunduliwa usiku wa Jumapili kuamkia Jumatatu katika eneo la Bihar, kaskazini mwa India. majimbo mengine manne ya India, Assam, Uttar Pradesh, West Bengal na Himalaya yameathirika, na katika jimbo pekee la Bihar, watu nusu milioni wameyahama makazi yao.
Nchini Nepal, Shirika la Msalaba Mwekundu lina wasiwasi kwamba uhaba wa maji safi na chakula unasababisha mgogoro mkubwa wa kibinadamu, hasa kwa kuwa maelfu ya wakazi walipoteza makazi yao.
Nchini Bangladesh, karibu watu milioni sita wamethiriwa na mvua hizo. Katika nchi zote tatu, mashirika ya kibinadamu yana hofu ya kuzuka kwa magonjwa kutokana na maji yaliyopo.
Wanyama pia wameathirika
Mafuriko pia yameathiri wanyama: katikajimbo la mashariki mwa India la Assam, asilimia 20 ya hifadhi ya wanyama ya Kaziranga inakabiliwa na maji. Wanyama mia mbili na ishirini na tano wamepatikana wamekufa. Miongoni mwao, faru kumi na tano, na viongozi wa hifadhi hii wana hofu kuwa majangili, wanaowinda faru hao kwa kuuza pembe zao, watanufaika na hali hiyo; Kwa hiyo zoezi la doria liliimarishwa na vizuizi vimewekwa katika maeneo yote ya hifadhi hiyo.
Kila mwaka, kimbunga hiki hupiga kusini mwa India mwanzoni mwa mwezi Juni hadi Asia ya Kusini kwa miezi minne, na kuua mamia ya watu.