Joe Biden aongelea kuhusu ung'atuzi unaomlenga Donald Trump
Makamu wa rais wa zamani na mgombea urais nchini Marekani ametangaza kwa mara ya kwanza kwamba anaunga mkono utaratibu ulioanzishwa na washirika wake kutoka chama cha Democratic katika Baraza la Wawakilishi.
Imechapishwa:
Joe Biden ni chanzo cha kesi ambayo ilipelekea kuzinduliwa kwa uchunguzi kuhusu ung'atuzi unaomlenga Rais Donald Trump. Rais wa Marekani alijaribu kupata habari za kutatanisha zenye lengo la kumtia matatani Joe Biden kutoka kwa mwenzake wa Ukraine. Makamu wa rais wa zamani anakabiliwa na tuhuma za kila mara kutoka kwa Donald Trump, ambaye amemhusisha na uvumi usio na msingi na kumtuhumu kwa madai ya ufisadi. Lakini Joe Biden mpaka sasa alikuwa amekataa kuzungumzia chochote kuhusu kung'atuliwa madarakani kwa Donald Trump. Hatimaye amebadilisha msimamo baada ya ikulu ya White House kutangaza kukataa kushirikiana na Bunge.
"Rais Trump amejishtumu mwenyewe. Kwa kuzuia mahakama kufanya kazi, kwa kukataa kutii hoja za Baraza la Wawakilishi, tayari amejihukumu mwenyewe. Mbele ya ulimwengu na raia wa Marekani, Donald Trump amekiuka kiapo chake, amesaliti taifa lake. Ili kulinda Katiba yetu, demokrasia yetu, kanuni zetu za msingi, anapaswa kufanyiwa uchunguzi ili aweze kung'atuliwa madarakani, "
Donald Trump amejibu mara moja kwenye ukurasa wake wa Twitter kuhusu hoja za mpinzani wake: alimwita Joe Biden kuwa mtu asiyefaa, na kuanzisha mashtaka mapya bila ushahidi.
Barua kutoka Ikulu ya White House kwa wabunge hao, ambao wengi ni kutoka chama cha Democratic, imesema uchunguzi huo hauna maana na ni kinyume cha katiba.
Trump amekuwa akisema kinachoendelea ni kumlenga na kumchafulia jina kuelekea uchaguzi Mkuu mwaka 2020.