Rais Trump azindua kampeni za kuwania urais kwa muhula wa pili
Rais wa Marekani Donald Trump amezindua rasmi kampeni za kuwania tena uongozi wa nchi hiyo kwa muhula wa pili, wakati wa Uchaguzi Mkuu mwaka 2020.
Imechapishwa:
Trump amewaambia maelfu ya wafuasi wa chama chake cha Republican mjini Florida kuwa waendelee kumuunga mkono anapoanza harakati za kupata uungwaji mkono wa chama chake cha Republican.
Aidha,Trump ameahidi kuwa hatawahi kuwaangusha wananchi wa Marekani.
“Usiku huu, nasimama mbele yenu kuzindua kampeni ya kuwania tena urais kwa muhula wa pili kuongoza Marekani, sitawahi kuwaangusha,” aliwaambia wafuasi wake waliokuwa wanamshangilia.
Aidha, alitumia uzinduzi huo kukikishtumu chama cha Democratic ambacho amedai kinajaribu kuiyumbisha nchi hiyo.
Mbali na rais Trump, wanasiasa wengine wa chama cha Republican ambao wameonesha nia ya kuwania urais ni pamoja na Gavana wa zamani wa jimbo la Massachusetts, Bill Weld
Wengine ni pamoja na Seneta wa zamani Bob Corker lakini pia aliyekuwa Gavana John Kasich.