Wizara ya Ulinzi ya Marekani yasema hakuna mpango wa kupigana na Iran
Wizara ya ulinzi nchini Marekani inasema msimamo wa rais Donald Trump kuhusu Iran, haimaanishi kuwa kutakuwa na vita kati yake na Iran kama ambavyo kiongozi wa nchi hiyo amekuwa akisema.
Imechapishwa:
Marekani kupitia naibu Waziri wa ulinzi Patrick Shanahan amesema msimamo wa Marekani ni kuzuia na sio kuanzisha vita.
"Marekani haitaki vita,"alieleza baada ya mkutano wake na Waziri wa mambo ya kigeni Mike Pompeo.
Iran na Marekani zimeendeleza vita vya maneno katika wiki za hivi karibuni wakati Marekani ikiimarisha vikwazo na kile inachosema ni lengo la kuishinikiza Iran kufanya makubaliano mengine mbali na masharti ya mkataba wake wa nyuklia wa 2015.
Aidha, ameeleza kile kilichofanywa na Marekani kuwa ni kuzuia mashambulizi dhidi ya mali na maslahi mengine muhimu kwa taifa hilo.
Naye Waziri wa mambo ya kigeni wa Iran Javad Zarif amesema hatua ya Marekani kuhamishia vifaa vya kijeshi katika ukanda wa ghuba ni kuhamasisha vita, na kuonya hatua hiyo inaongeza hatari ya 'ajali' kutokea.