Nikki Haley ajiuzulu kuwa Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa
Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Nikki Haley ametangaza kujiuzulu, baada ya kuhudumu katika nafasi hiyo kwa karibu miaka miwili.
Imechapishwa:
Haley mwenye umri wa miaka 46 hajasema ni kwanini ameamua kujiuzulu na kukanusha madai kuwa amefanya uamuzi huo ili kuwania urais mwaka 2020.
Rais Donald Trump amesema amekubali uamuzi wake na kumsifia kwa kufanya kazi nzuri aliyofanya katika Umoja huo.
Aidha, Trump amesema kuwa Balozi mpya atateuliwa baada ya wiki tatu.
“Aliniambia miezi sita iliyopita kuwa, anataka kupumzika,” alisema rais Trump baada ya kukutana na Haley katika Ikulu ya White House.
Gavana huyo wa zamani wa jimbo la South Carolina, aliteuliwa na rais Trump kushika nafasi hiyo, akiwa hana uzoefu mkubwa wa mambo ya nje lakini, kazi yake imesifiwa na kila mmoja.
Licha ya kuondoka, Haley amesema ataendelea kumheshimu rais Trump.