Rais Trump amfuta kazi Tillerson, amteua Mike Pompeo
Rais wa Marekani Donald Trump amemfuta kazi Waziri wake wa Mambo ya nje Rex Tillerson na kumteua Mkurugenzi Mkuu wa CIA Mike Pompeo kuchukua nafasi hiyo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
“Mike Pompeo, Mkurugenzi wa CIA, atakuwa Waziri wetu mpya wa Mambo ya nje. Atafanya kazi nzuri,” Trump ameandika kupitia ukurasa wake wa Twitter.
“Asante sana Rex Tillerson kwa huduma yako,” aliongeza rais Trump.
Aidha, amesema kuwa alitofautiana na Tillerson kuhusu baadhi ya masuala hasa kuhusu mkataba wa Iran, kati ya nchi hiyo na nchi za Magharibi.
"Namtakia Tillerson kila la heri, amekuwa mtu mwema sana," alisema Trump.
Hatua hii imekuja baada ya Tillerson kumaliza ziara yake barani Afrika baada ya kuzuru Ethiopia, Kenya, Chad, Djibouti na Nigeria.
Hata hivyo, Tillerson alisitisha ziara yake barani Afrika baada ya kusema kuwa alikuwa na mambo muhimu ya kwenda kufanya jijini Washington DC.
Yote haya yanakuja wakati huu rais Trump akitarajiwa kukutana na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jonn Un mwezi Mei mwaka huu kujadili mradi wake wa nyuklia.
Ripoti zinasema kuwa, Trump alimwarifu Tillerson Ijumaa iliyopita kuwa alikuwa anakwenda kumbadilisha katika nafasi hiyo, lakini hakupewa sababu yoyote.
Wachambuzi wa siasa za Kimataifa wanasema kwa kiasi kikubwa, uamuzi wa Trump umekuja kutokana na mkutano unaopangwa hivi karibuni kati ya kiongozi wa Marekani na Korea Kaskazini.
Kabla ua uteuzi wake, Tillerson alikuwa mfanyibiashara na Mwenyekiti wa kampuni ya mafuta na gesi ya ExxonMobil, nafasi aliyohudumu kwa muda mrefu.
Mike Pompeo ambaye ni mwananasiasa na afisa wa juu wa Intelejensia nchini Marekani, anatarajiwa kutumia uzoefu wake kumsaidia rais Trump katika utekelezaji wa sera yake ya mambo ya nje.
Kazi ya kuongoza CIA, sasa imemwendea Gina Haspel ambaye alikuwa naibu wa Pompeo.
Haspel anakuwa mwanamke wa kwanza katika historia ya Marekani kuongoza kitengo hicho cha ujasusi nchini Marekani.