Pata taarifa kuu
MAREKANI-ISRAEL-PALESTINA

UN: Trump atishia kusitisha misaada kwa nchi zitakazopiga kura dhidi yake

Rais wa Marekani Donald Trump ametishia kusitisha misaada ya kifedha kwa mataifa yatakayounga mkono azimio la umoja wa Mataifa linalolenga kutotambua uamuzi wa nchi yake kutambua mji wa Jerusalem kama makao makuu ya Israel.

Donald Trump rais wa Marekani
Donald Trump rais wa Marekani REUTERS/Yuri Gripas
Matangazo ya kibiashara

Rais Trump alikuwa akizungumza mjini Washington wakati akisifu namna wabunge wake walivyopitisha mabadiliko ya mfumo wa kodi, lakini akagusia suala la nchi yake kuutambua mji wa Jerusalem.

Trump sasa anasema nchi zitakazopiga kura kuunga mkono azimio hili la umoja wa mataifa zijiandae kwa kulipa gharama ya kura yao.

Matamshi ya Trump yanakuja saa chache kabla ya baraza la nchi wanachama za umoja wa mataifa kupigia kura azimio linalopinga kutambuliwa kwa Jerusalem kama makao makuu ya Israel.

Nikki Haley balozi wa Marekani kwenye umoja wa Mataifa
Nikki Haley balozi wa Marekani kwenye umoja wa Mataifa Drew Angerer / GETTY IMAGES NORTH AMERICA / AFP

Juma hili wakati wa kikao cha baraza la usalama la umoja wa Mataifa Marekani ilitumia kura yake ya turufu kukwamisha azimio lililokuwa limewasilishwa na Misri kutaka kuzuia uamuzi wa Marekani kutambua mji wa Jerusalem kama makao makuu ya Israel.

Hata hivyo Misri pamoja na mamlaka ya Palestina ziliamua kuendelea mbele na azma yao ambapo wamewasilisha azimio lao kwenye mkutano wa nchi wanachama wa baraza la umoja wa Mataifa ambako hakuna kutumia kura ya turufu.

Kinachosubiriwa sasa ni kuona ikiwa nchi zilizotishiwa zitapiga kura kuidhinisha azimio hilo la umoja wa Mataifa.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.