Trump na Waziri Mkuu wa Australia wajibizana vikali
Gazeti maarufu la Marekani la The Washington Post, limeripoti kuwepo kwa majibizano makali kati ya rais wa Marekani Donald Trump na Waziri Mkuu wa Australia Malcolm Turnbull.
Imechapishwa:
Ripoti zinasema kuwa viongozi hao wawili walikuwa wanazungumzia mkataba uliofikiwa kati ya Australia na rais wa zamani Barack Obama kuhusu makubaliano ya wakimbizi 1, 250 kupewa hifadhi nchini Marekani.
Wakimbizi hao ni kutoka Iran, Afganistan na Iraq na inakuja baada ya rais Trump kuwazuia raia wa mataifa saba ya Kiislamu kuingia nchini humo.
Mwezi Novemba mwaka uliopita, Australia ilitangaza kuwa ilikuwa imefikia mwafaka huo na Marekani kuwachukua wakimbizi hao wanaoishi katika visiwa vya Nauru na Manus katika eneo la Papua New Guinea.
Rais Trump ameendelea kushtumiwa kote duniani kwa sera yake ya kuwakataa wakimbizi hasa kutoka mataifa ya Kiislamu kwa kile kinachoelezwa kuwa ni ubaguzi.