Colombia: Serikali na waasi wa FARC kutia saini mkataba mpya wa amani
Serikali ya Colombia na waasi wa kundi la FARC, watatia saini mkataba mpya wa amani Alhamisi ya wiki hii, baada ya ule mkataba wa awali kukataliwa na wananchi katika kura ya maoni, mkataba unaolenga kumaliza mzozo uliodumu kwa karibu nusu karne.
Imechapishwa:
Rasimu mpya ya mkataba wa amani, itawasilishwa kwenye baraza la Congress kwaajili ya kuidhinishwa, ambapo sasa Serikali imekwepa kufanya kura nyingine ya maoni, imesema taarifa ta wapatanishi wa mzozo huo.
Mwezi uliopita, wananchi walioshiriki kwenye kura ya maoni, waliukataa mkataba wa amani uliotiwa saini kati ya Serikali na waasi wa FARC, wadadisi wa mambo wakisema kuwa, waasi walionewa huruma sana, wakati wametekeleza makosa ya uhalifu wa kivita.
"Serikali na wajumbe wa kundi la FARC wamekubaliana kutia saini makubaliano ya mwisho ili kumaliza mzozo uliodumu kwa miongo kadhaa na kuijenga nchi hiyo upya kupitia maridhiano," wamesema wapatanishi kutoka pande zote mbili.
Mkataba mpya wa amani ulitangazwa kwa mara ya kwanza mwezi Novemba 12 na sherehe za utiaji saini zitafanyika mjini Bogota, Alhamisi ya wiki hii.
Mkataba huu sasa utawasilishwa kwa baraza la Congress kwaajili ya kupigiwa kuwa, mkataba ambao sasa huenda ukapitishwa hasa kutokana na ukweli kuwa, baraza la Congress lina wajumbe wengi wa chama tawala.
Rais wa Colombia Juan Manuel Santos, amesisitiza kuwa mapendekezo mapya ni muhimu na yamezingatia pia mapendekezo yaliyotolewa na vyama vya upinzani ambavyo vilipinga mkataba huo.