Mwaka mmoja wa Ebola DRC: Juhudi za kupambana na Ebola zakabiliwa na changamoto mbalimbali
Ni mwaka mmoja sasa, baada ya kuripotiwa kwa maambukizi ya Ebola Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, maambukizi ambayo yameendelea kuzua wasiwasi miongoni mwa wakaazi wa Beni, Ituri na sasa Goma.
Imechapishwa:
Julai 31 mwaka uliopita, maafisa wa afya Mashariki mwa DRC, maafisa wa afya waliripoti kuwa watu wanne walikuwa wameambukizwa ugonjwa huo hatari katika jimbo la Kivu Kaskazini.
Wiki mbili baadaye, mtu mwingine aliambukizwa katika mkoa wa Ituri.
Kufikia mwezi Novemba mwaka 2018, Shirika la Afya Duniani WHO lilitangaza kuwa maambukizi hayo yalikuwa mabaya kuwahi kushuhudiwa katika historia ya nchi hiyo ya Afrika ya Kati.
Kwa kipindi hiki cha mwaka mmoja, maambukizi ya Ebola yameripotiwa hasa katika maeneo ya Beni, Butembo, Oicha, Musienene na Mabalako katika mkoa wa Kivu Kaskazini, huku maeneo ya Mandima na Mambasa yakiathiriwa katika Jimbo la Ituri.
Hadi sasa, shirika la Afya Duniani, WHO, linasema kuwa ugonjwa huu umekuwa janga la Kimataifa, huku Umoja wa Mataifa ukisema fedha zaidi zinahitajika ili kupambana na maambukizi haya.
Mwaka mmoja baadaye watu 1,803 wamepoteza maisha huku wengine zaidi ya 2,000 wakiambukizwa, na kuwepo pia kwa makundi ya waasi yakielezwa kutatiza juhudi za kumaliza maambukizi haya kwa sababu yameendelea kushambulia vituo vya afya.