Mafuriko DRC: Idara ya Mipango Miji ya Kinshasa yanyooshewa kidole cha lawama
Takriban watu 41 walifariki dunia usiku wa Jumatatu kuamkia Jumanne, haswa katika Wilaya za Lemba na Mont Ngafula, kwenye milima ya mji mkuu Kinshasa.
Imechapishwa:
Mamlaka inatarajia kubomoa nyumba zilizojengwa kimakosa katika maeneo yenye mafuriko, lakini manusura hawatoondoka maeneo hayo bila kulipiwa bima.
Wakazi wengi wa maeneo yaliyoathiriwa na mafuriko katika mji wa Kinshasa wameishtumu idara ya Mipango Miji kwamba imechangia kwa njia moja ama nyingine kwa hali hiyo iliyoukumba maeneo yao.
Baadhi ya wakazi wa maeneo yaliyoathirika wameendelea kuomba misaada kutoka kwa serikali na mashirika ya kihisani, huku wengi wao wakilala nje.
Wengi wamesema wameshindwa kulala wakifikiria hali iliyokumba maeneo yao.
Ili kuondoka katika makazi yao, wengi wametoa masharti na kutaka kujua iwapo serikali itawasaidia kwa kuwajengea makaazi mapya.
"Tutwende wapi hasa? Serikali lazima itusaidie kwa kukarabati maeneo mengine na kutusaidia katika ujenzi wa makazi mapya. La sivyo, tutakubali kupoteza maisha, " mmoja wa wakazi hao amesema.
Wataalamu, wamehoji tabia ya kutotii sheria za mipango miji.