Watu 3 wauawa katika shambulio la kuvizia Eringeti, DRC
Watu watatu wameuawa na saba kujeruhiwa baada ya kushambuliwa na watu wenye silaha katika eneo la Eringeti, huko Beni Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Imechapishwa:
Ripoti zinasema kuwa, wapiganaji wa ADF Nalu waliwashambulia kwa risasi watu waliokuwa wanatoka sokoni katika mji wa Oicha.
Hali hii inajiri wakati hivi majuzi rais wa jamhuri ya kidemokrasia ya Congo Felix Tshisekedi akizindua Operesheni za kijeshi katika kupambana na waasi wa ADF huku akisema kuwa amepata uungwaji mkono wa serikali ya Marekani, na baadhi ya nchi jirani katika kutoa ushirikiano wa karibu kupambana na makundi ya wapiganaji kwenye eneo la Mashariki mwa nchi hiyo.
Katika hatua nyingine polisi wa DRC waliopelekwa mjini Beni na viunga vyake wamekabidhiwa vifaa vipya maalum katika kukabiliana si tu na waasi lakini pia raia watakaothubutu kuendeleza maandamano ya kupinga shughuli za serikali kwenye maeneo hayo.