Koffi Olomide: Naonewa na serikali, nyimbo zangu zimezuiwa
Mwanamuziki Koffi Olomide anayeimba nyimbo aina ya Soukus kutoka nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ameishtumu serikali ya nchi hiyo kwa kuzuia nyimbo zake nane, kitendo ambacho anasema ni ukiukwaji mkubwa wa haki zake za kujieleza.
Imechapishwa:
Cheza - 02:38
Olomide amemwambia mwandishi wetu wa Kinshasa Freddy Tendilonge katika mazungumzo kuwa, hatua iliyochukuliwa na kamati ya serikali inayosimamia maudhui ya wanamuziki haikubaliki.
“Tatizo ni nini ? Kabla ya kuimba ni lazima uende kwa watu hao, mimi sitakubali hili, siwezi kwenda kuwapigia magoti,” alisema Koffi.
“Najiuliza hawa watu wananilenga mimi Koffi au wanaangalia maudhui ya nyimbo zangu,” ? aliuliza.
Aidha, amewaambia mashabiki wa muziki wake kuendelea kushinikiza kuondolewa kwa marufuku hayo, na kutoa wito kwa rais Felix Tshisekedi kuingilia kati suala hili.
“Nawaomba raia wote wa DRC kusimama pamoja na kuipinga Kamati hii, ambayo iliundwa miaka zaidi ya 40 iliyopita na Marehemu Mobutu, namwomba rais Tshisekedi aingilie kati kwa sababu aliahidi usawa na demokrasia alipoingia madarakani,” aliongeza.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Bernadin Mayi-Ndombe amekanusha madai ya Olomide na kusema kuwa inafuata sheria wala haimlengi mwanamuziki huyo.