Umoja wa Mataifa kuendelea kuwa nchini Libya kwa mwaka mmoja zaidi
Baraza la Usalama la umoja wa Mataifa limeongeza kwa muda wa mwaka mmoja, ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Libya, katika jitihada za kuhimiza amani na kusaidia kuleta udhabiti wa kisiasa nchini humo.
Imechapishwa:
Hatua hii inakuja, baada ya mjumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Libya Ghassan Salamé, kuonya kuwa huenda nchi hiyo itagawanyika mara mbili iwapo amani ya kudumu haitapatikana haraka iwezekanavyo.
Aidha, ameonya kuwa kuendelea kwa vita nchini Libya, kunachangiwa na mataifa ya nje yanayounga mkono makundi mawili yanayopigana katika nchi hiyo ya Afrika Kaskazini.
Wanajeshi wa Serikali inayotambuliwa na Umoja wa Mataifa, yenye makao yake jijini Tripoli, wamekuwa wakipambana na wapiganaji wa Jenerali Khalifa Haftar wanaodhibiti eneo la Mashariki mwa nchi hiyo.
Pande zote mbili zinapata silaha kutoka kwa washirika wao licha ya vikwazo vya Umoja wa Mataifa, kuzuia uingizwaji wa silaha katika taifa hilo.
Jenerali Haftar ameendelea kupata msaada wa silaha kutoka kwa Ufaransa, Marekani na Urusi licha ya azimio la Umoja wa Mataifa kutaka mataifa hayo kuacha kuingilia mzozo huo.