Umoja wa Afrika walaani chuki dhidi ya wageni Afrika Kusini
Umoja wa Afrika umelaani chuki dhidi ya wageni na kusababisha ghasia nchini Afrika Kusini. Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika Moussa Faki, amelaani ghasia hizo lakini akaongeza kuwa ametiwa moyo na hatua zilizochukuliwa na Afrika Kusini za kuwakamata watuhumiwa.
Imechapishwa:
Wakati huo huo shirikisho la mpira wa miguu la Zambia FAZ, limefuta mechi ya kirafiki iliyokuwa ifanyike mjini Lusaka siku ya Jumamosi kutokana na vurugu hizo. Kwenye taarifa yake iliyoitoa Jumanne, FAZ imesema sababu za kusitisha mechi hiyo ni hali ya kiusalama nchini Afrika Kusini, hata kama Zambia ilikuwa mwenyeji.
Hadi kufikia sasa watu watano wamepoteza maisha kutokana na ghasia hizo, na polisi wamewakamata zaidi ya watu 80 kuhusiana na matukio hayo ya chuki dhidi ya wageni,
Kwa upande wake Nigeria imemwita balozi wa Afrika Kusini nchini humo na kutuma ujumbe mjini Pretoria ili kuelezea masikitiko makubwa dhidi ya raia wake kushambuliwa.
Rais Muhammadu Buhari amechukua hatua hiyo kufuatia makundi ya raia wa Afrika Kusini kuvamia biashara katika sehemu tofauti za nchi hiyo, wakipora mali na kuchoma magari katika wimbi jipya la chuki dhidi ya wageni.
Serikali ya Nigeria kupitia Ukurasa wake wa Twitter iliandika kwamba ujumbe wake utawasili mjini Pretoria siku ya Alhamis na kukutana na rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa.
Rais Cyril Ramaphosa amelaani mashambulizi dhidi ya wageni na uvamizi wa maeneo yao ya biashara jijini Johhanersburg.
Kiongozi huyo kupitia ujumbe aliotuma kwenye ukura wake wa Twitter, amesema mashambulizi hayo hayakubaliki.